KIBOKO YA JOHN BOCCO YUPO TAYARI YANGA

 

DICKSON Job, beki wa kazi ndani ya kikosi cha Yanga kinachonolewa na Kocha Mkuu, Nasreddine Nabi yupo kamili gado kwa ajili ya kuwavaa Simba kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara unaotarajiwa kuchezwa Desemba 11, Uwanja wa Mkapa.

Job anakumbukwa na mshambuliaji bora wa msimu wa 2020/21 John Bocco aliyefunga mabao 16 kwa namna alivyoweza kumdhibiti ili asiwafunge kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii uliochezwa Uwanja wa Mkapa, Septemba 25.

Job alipata maumivu kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mbeya Kwanza uliochezwa Uwanja wa Sokoine Septemba 30 jambo lilomfanya akwame kumaliza dakika 90.

Mtu wa karibu wa Job amesema kuwa mchezaji huyo yupo tayari kwa ajili ya mchezo huo na anasubiri kuona akipewa nafasi na Kocha Mkuu, Nasreddine Nabi kuweza kuanza kikosi cha kwanza.

“Nabi kwa sasa anajua nani atamtumia kwenye mchezo huo lakini ukweli ni kwamba Job yupo tayari ni suala la kusubiri na kuona namna mambo yatakavyokuwa,”.

Nabi amesema kuwa wachezaji wake wote wapo tayari kwa mchezo huo jambo ambalo linampa nafasi ya kuweza kuchagua kikosi imara cha ushindi.

“Wachezaji wapo tayari na nimewaambia kwamba kila mchezaji ana nafasi ya kuanza kikosi cha kwanza ndio maana kuna wakati kunakuwa na mabadiliko hivyo ninachoweza kusema ni kwamba wachezaji wote watacheza.

“Kuelekea mechi yetu dhidi ya Simba tupo tayari na tunawaheshimu wapinzani wetu. Mimi ni mtu wa mpira na ninajua sipendi kuongea sana ila nitaongea kwa vitendo,” alisema Nabi.

Chanzo:Championi

Previous Post Next Post

Translate